Kwanzaa

From Wikipedia

Mwanamke anawasha mshumaa wa kinara. Kuna ishara nyingi ya Kwanzaa mezani.
Mwanamke anawasha mshumaa wa kinara. Kuna ishara nyingi ya Kwanzaa mezani.

Kwanzaa ni sikukuu inayosherehekewa na Wamarekani Weusi na watu wengine wenye asili ya Afrika sehemu mbalimbali duniani. Kwanzaa husherehekewa kwa siku saba toka Desemba 26 hadi Januari 1. Sikukuu hii iliyotokana na vuguvugu la watu weusi nchini Marekani kuenzi historia na utamaduni wao toka Afrika ilianzishwa na Dakta Maulana Karenga Desemba 26, 1966.

Neno "Kwanzaa" limetokana na neno la Kiswahili "Kwanza." Herufi "a" iliongezwa katika neno hilo ili kulifanya neno hilo kuwa na herufi saba, sawa na idadi ya siku za kusherehekea sikukuu hii. Baadhi ya watu weusi huchukulia sikukuu hii kuwa na umuhimu sana kwao kama vile ilivyo Hannuka kwa Wayahudi au Krisimasi kwa Wakristo. Kutokana na nia ya kuenzi Uafrika, Kiswahili hutumika katika sikukuu hii.

Sherehe hii imejengwa juu ya maadili ya kitamaduni ya Kiafrika na huchukuliwa kuwa ni kama aina za sherehe za makabila mbalimbali Afrika wakati wa mavuno. Maadili haya ya Kiafrika yamegawanywa katika dhana iitwayo Nguzo Saba. Kwa siku saba, kila siku huwa na nguzo yake ya kukumbuka na kuenzi. Nguzo hizo ambazo zinafahamika kwa Kiswahili ni: Umoja, Kujichagulia, Ujima, Ujamaa, Nia, Kuumba, na Imani. Nguzo saba hizi hutumiwa kama moja ya njia ya kuimarisha umoja wa kifamilia miongoni mwa jamii za Wamarekani Weusi na pia njia ya kuwakumbusha historia na utamaduni wao.

Sikukuu hii inatumia alama kadhaa ambazo nazo zinatambulika kwa lugha ya Kiswahili. Alama hizo ni:

  • Mazao
  • Mkeka
  • Kinara
  • Muhindi
  • Mishumaa Saba
  • Kikombe cha Umoja
  • Zawadi

Kati ya shughuli zinazofanywa wakati wa sikukuu hii ni kuwasha mishumaa saba (mshumaa mmoja kila siku) na kutoa tambiko la kuenzi wmababu na mabibi waliotangulia. Mishumaa hii huwa ina rangi za kijani, nyekundu na nyeusi. Mshumaa mweusi huwekwa katikati na ndio huwa wa kwanza kuwashwa. Huwashwa siku ya kwanza. Rangi nyeusi huwakilisha watu weusi, rangi nyekundu hukumbusha mapambano na masahibu yaliyowakumba walitangulia, na rangi ya kijani humaanisha utajiri wa bara la Afrika na pia matumaini mema ya watu weusi.

[edit] Viungo vya nje