Dini ya kiislamu

From Wikipedia

Unganisha! Imependekzwa makala hii iunganishwe na Uislamu. (Jadili)
Kuna mashaka kuhusu baki ya makala hii. Uone majadiliano.

Dini ya kiislamu ni mfumo wa maisha ambao Mwenyezi Mungu amewawekea wanadamu ili waishi maisha mazuri hapa duniani na wapate radhi za Mola wao kesho Akhera. Mfumo huu umekusanya kila linalohusu aina mbali mbali ya nidhamu ya maisha, kama nidhamu ya jamii, siasa, uchumi, na maingiliano mengineo baina ya wanadamu kwa jumla.

Kutokana na mfumo huu, mwanadamu anaweza kuishi kwa raha na amani na wenzake ulimwenguni, na kuwa katika hali ya furaha daima, maadamu anafuata maelekezo ya Mola wake, na kutekeleza maamrisho waliyokuja nayo Mitume na Manabii katika zama mbali mbali. Mfumo huu wa maisha akiufuata vilivyo, unampa utulivu na amani katika uhai wake hapa duniani na unampa kufuzu kukubwa kesho Akhera.

Dini katika Uislamu, si kitu mbali na maisha ya binadamu, kwani inamuongoza namna gani kumuabudu Mola wake inavyotakikana, na namna gani kuishi na wenzake bila ya kuudhiana. Nayo hunadhimu maisha yake ya kiroho na kiwiliwili, na kuweka mizani baina ya aina mbili hizi za maisha, ili asipate taabu hapa duniani wala kesho Akhera.

Dini ya Uislamu inagusia kila sehemu ya maisha ya mwanadamu, na inatoa muongozo katika kila jambo, ili mwanadamu awe khalifa na mwakilishi mzuri wa Mola wake hapa ulimwenguni, kwani yeye ameletwa hapa duniani aishi akimuabudu Mola wake, na akae na wenzake kwa wema na hisani, na kuingiliana nao kwa kila njia nzuri na ya kheri.

Kwa hivyo, tunaona katika Uislamu kuna nidhamu ya kijamii inayohusu ndoa na talaka na nafaka na mirathi na arusi na mazishi, na kila linalohusu jamii. Aidha, tunaona kuna nidhamu ya uchumi, na namna gani kufanya biashara na kukuza mali na kukopa na kulipa, kama vile vile tunavyoona nidhamu ya kivita wakati maadui wanapotaka kuleta mchafuko katika nchi, na jihadi dhidi ya wanaomuasi Mwenyezi Mungu.

Nidhamu ya ibada, pia ina mipango yake. Maana kuna Sala na Saumu na Zaka na Hija, na kila moja katika ibada hii ina namna zake na masharti yake na wakati wake. Nalo hili la ibada linadumisha uhusiano baina ya mwanadamu na Mola wake, na kuzidi kumkurubisha baina yake na Mola wake.

Kwa ufupi, dini ni jambo la dharura sana kwa mwanadamu, kwani bila ya dini, mara nyingi mwanadamu hurudi akawa mshenzi na kufanya mambo yasiyokuwa laiki kwa binadamu kwa kutofahamu uhusiano wake na Mola wake, na huwa duni kuliko mnyama.