Papa Gregori XIII
From Wikipedia
Papa Gregori XIII (*7 Januari 1502 mjini Bologna/Italia †10 Aprili 1585 Roma) alikuwa papa wa kanisa katoliki kati ya 1572 hadi 1585.
Anakumbukwa hasa kwa matengenezo ya kalenda iliyojulikana kama "kalenda ya Gregori" ikawa kalenda ya kimataifa kote duniani.
Alizaliwa kwa jina la Ugo Buoncampagni akafuata masomo ya sheria na kuwa profesa ya sheria kwenye chuo kikuu cha Bologna. Mwaka 1539 aliitwa na kanisa akapewa kazi mbalimbali kwama mwanasheria wa kanisa. Papa Paulo IV alimpa cheo cha askofu wa Viesti (Italia) na ni sasa tu ya kwamba Ugo alikula kiapo cha upadre na kubarikiwa kama askofu mara moja.
Baada ya kifo cha Papa Paulo IV alichaguliwa kuwa mfuasi wake akachukua jina la "Gregorius". Papa Gregori VII alijitahidi kurudisha nyuma mwendo wa matengenezo ya kiprotestant. Alikubali kudhulumiwa kwa Wainjili nchini Ufaransa tar. 23 -24 Agosti 1572 ("Usiku wa Bartolomeo"). Alijaribu kukusanya mataifa ya Ulaya dhidi ya Dola la Uturuki kwa shabaha ya kukomboa mji wa Konstantinopoli lakini hakufaulu.
Pamoja na jitihada hizi za kisiasa alijenga taasisi ya taaluma. Aliunda Chuo Kikuu cha Mapapa huko Roma kinachoitwa kwa heshima yake "Gregoriana" hadi leo.
Kalenda mpya hakutunga lakini aliita wataalamu katika kamati maalumu na kukubali mapendekezo yake tar. 24 Februari 1582.