Mwenyezi Mungu

From Wikipedia

Neno Mwenyezi Mungu kwa lugha ya Kiswahili linatumika kwa Muumba wa kila kitu, Mwenye kuabudiwa kwa haki, kinyume na neno 'mungu' ambalo lina maana chochote au yeyote anayeabudiwa ikiwa kwa haki au si kwa haki. Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu ni Muumba wa mbingu na ardhi na kila kilichomo baina yake, naye ni Mlezi wa viumbe vyote na Mpaji riziki kwa kila chenye uhai ulimwenguni.

Mwenyezi Mungu, katika dini na mila nyingi duniani, ni yule anayestahiki kuabudiwa kwa haki ikiwa peke yake bila kushirikishwa na chochote, au kwa kushirikishwa na viumbe vyengine, kwa nia ya kuwa hawa viumbe vyengine vinamkurubisha naye. Hii ni kwa sababu, kila dini au mila ina namna yake ya kumsawiri Mwenyezi Mungu, na njia gani sahihi ya kumuabudu, na kwa kuwa hakuna itifaki baina ya hizi dini, mila na madhehebu kuhusu Mwenyezi Mungu na namna anavyotakikana kuabudiwa, hizi tofauti chungu nzima zimetokea.

Contents

[edit] Imani ya Waislamu

Uislamu, kwa mfano, unaeleza kuwa Mwenyezi Mungu ni Mmoja tu hana mshirika, hana mwanzo wala mwisho, hakuzaa wala hakuzaliwa, na wala hapana yeyote mwenye kufanana au kushabihiana naye, naye ni Mola wa ulimwengu huu wote, na Muumba wa kila kitu. Kwake Yeye inatoka riziki ya kila kiumbe, na Yeye ndiye Mwenye kuhuisha na Mwenye kufisha. Marejeo ya viumbe vyote wakishakufa na kufufuliwa ni kwake Yeye tu siku ya Kiyama. Yeye pekee ndiye Mwenye kuhukumu viumbe siku ya malipo, na ndiye atakayewapa waja wake ujira na thawabu na kuwatia Peponi kwa mema waliyoyafanya, au kuwatia adabu na kuwapa adhabu na mateso na kuwatia Motoni kwa maovu waliyotenda hapa duniani.

[edit] Imani ya Wakristo

Ukristo unakubaliana na Uislamu katika mengi ya sifa hizi za Mwenyezi Mungu za kuumba, kuhuisha na kufisha, kuruzuku, kufufua, kuhukumu na kulipa ya kheri kwa mwenye kufanya kheri na ya shari kwa mwenye kufanya shari, lakini aghlabu ya madhehebu za Kikristo, ijapokuwa si zote, zinampa Mwenyezi Mungu sifa ya utatu, na kumsifu kuwa ni Mungu Baba, na Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu, na kuwa wote hawa watatu wanashirikiana katika Uungu na kuwa ni kitu kimoja. Uislamu, kwa upande wake, unakataa katakata mas-ala ya kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu chochote, na kwa hivyo ni Mmoja tu wala hana mshirika wa aina yoyote.

[edit] Dini nyinginezo

Dini nyenginezo, kadhalika, zina tasauri na fikra nyengine kuhusu Mwenyezi Mungu. Kuna wale wanaoabudu viumbe mbali mbali wakichukulia kuwa wanamwakilisha Mwenyezi Mungu, kama kuabudu masanamu, nyota, jua, ngo'mbe, wanyama mbali mbali, mizimu, miti, panya, moto, viumbe wenziwao, malaika na majini na kadhalika. Dini na mila hizi, pengine huchukulia kuwa vitu hivi vinatusaidia kutufikisha kwa Mwenyezi Mungu, na kuwa bila ya vitu hivi, ibada zetu haziwezi kufika. Ama wengine huwa na imani kuwa vitu hivi ndio Mola mwenyewe wa kuabudiwa na kuombwa na kutakwa msaada.

[edit] Sifa za Mwenyezi Mungu

Kama tulivyoeleza, Mwenyezi Mungu ana sifa mbali mbali kwa mujibu wa dini na mila na madhehebu tofauti tofauti, na kila watu wanamsifu Mwenyezi Mungu kwa namna ambayo wanavyomjua wao kulingana na mafunzo ya dini na mila zao. Hii ni kwa sababu, watoto tangu wazaliwapo hufunzwa na wazee wao habari za Mwenyezi Mungu na namna ya kumuabudu, na mafunzo haya hubakia katika mawazo na fikra zao, na kukuwa nayo mpaka ukubwani mwao.

[edit] Mwenyezi Mungu kwa Waislamu

Waislamu, wanafunzwa tangu utotoni mwao kuwa Mwenyezi Mungu ni Mmoja tu peke yake, hana mshirika naye ndiye mwenye kufaa kuabudiwa kwa haki bila ya kushirikishwa na chochote katika viumbe vyake na kuwa Yeye ni wakutegemewa katika kila kitu na kuombwa msaada na kuombwa msamaha wakati wa makosa na madhambi. Yeye hana kitu kilichofanana naye, hakuzaa wala hakuzaliwa, hana mwanzo wala mwisho. Mwingi wa rehema na Mwenye kurehemu, Mtoa riziki, Mwenye kuhuisha na Mwenye kufisha. Hukumu yote ni yake siku ya Kiyama. Mtukufu na Mkubwa. Bwana na Mola wa walimwengu wote. Yeye tu ndiye Mwenye kustahiki kuabudiwa na Yeye tu ndiye Mwenye kufaa kuombwa na kutakwa msaada.