Kyrilo wa Saloniki
From Wikipedia
Mtakatifu Kyrilo (kigir. Κύριλλος (kyrillos), Kikyrili Кирилъ; * 826/827 mjini Thessaloniki; † 14 Februari 869 mjini Roma) alikuwa mmonaki na mtaalamu wa Kigiriki aliyeweka msingi kwa ajili ya utamaduni wa kikristo kati ya mataifa ya Waslavoni.
Alizaliwa kwa jina la "Konstantino" mjini Thessaloniki au Saloniki katika Ugiriki ya kaskazini wakati wa enzi za Dola la Bizanti kama mtoto wa askari wa Kibizanti na mke wake Mslavoni.
Jina la "Kyrilo" alipokea baada ya kujiunga na monasteri ya Kigiriki.
[edit] Kijana na elimu
Alipokea mafunzo yake ya ngazi ya juu kwenye chuo kikuu cha mji wa Konstantinopoli katika masomo ya falsafa, sarufi, mahubiri, muziki, mahesabu, jiografia na astronomia. Alijifunza pia lugha za Kigiriki, Kilatini, Kisiryani na Kiebrania. Baadaye aliongeza Kiarabu. Lahaja za Kislavoni alijua tangu utoto.
Mnamo mwaka 848 alijiunga na utumishi wa kanisa akapokea baraka za dikoni. Katika mapokeo ya kanisa la kiorthodoksi angeruhusiwa kufunga ndoa hata kama kasisi wa kanisa lakinim aliamua kufuata mtindo wa wamonaki. Manmo 850 alipewa kazi ya kufundisha falsafa kwenye chuo kikuu cha Konstantinopoli.
[edit] Safari kwa Waarabu na Wakhazari
Mnamo mw. 851 alitumwa kama balozi wa Kaisari kwenda Samarra na ujumbe kwa Khalifa Al-Mutawakkil alipoingia katika majadiliano na wataalamu Waislamu kuhusu Mungu na dhana ya utatu.
Alifanya bado safari nyingine kubwa kwenda kwa Wakhazari waliokuwa Waturuki waliofuata imani ya Kiyahudi katika maeneo kaskazini ya Bahari Nyeusi.
[edit] Safari kwenda Moravia kati ya Waslavoni
Mwaka 862 Rastislavo mtawala wa Waslavoni katika Moravia alimwomba Kaisari Michael III. Konstantino wa Konstantinopoli kumtuma "askofu na mwalimu" atakayefundisha watu wa kawaida katika Ukristo kwa lugha ya watu. Inaaminiwa ya kwamba Ratislav alitaka kujenga Ukristo na kanisa nchini yake bila kutegemea majirani Wajerumani waliowahi kujenga misingi ya Ukristo katika Moravia. Hivyo alitafuta uhusiano na Bizanti iliyofuata mtindo tofauti wa Ukristo haikuwa chini ya Papa wa Roma.
Kaisari alimtuma Kyrilo pamoja na kakaye Methodio kwa sababu wote wawili walikuwa watu wa kanisa wenye elimu nzuri wakijua lugha ya Kislavoni tangu utoto.
Tangu mwaka 863 Kyrilo na Methodio waliisha na kufanya kazi kati ya makabila ya Waslavoni. Walitafsiri sehemu za Biblia hasa Agano Jipya na liturgia katika lugha ya watu. Walifaulu hata kupata kibali cha Papa wa Roma kwa matumizi ya Kislavoni kanisani. Waliunda aina ya lugha inayojulikana kama "Kislavoni cha kanisa" inayoendelea kutumiwa hadi leo katika liturgia ya Wakristo waorthodoksi Urusi, Serbia na Bulgaria.
Kwa kazi yao walianzisha aina ya mwandiko wa pekee iliyokuwa chanzo cha alfabeti inayoitwa hadi leo "Kikyrili" kwa hesima ya Kyrilo.
Kwa shughuli zao Kyrilo pamoja na Methodio walieneza Ukristo na kuweka msingi kwa utamaduni wa kikristo kati ya mataifa ya Kislavoni ya leo.